Main Article Content
Abstract
Mabango ni mojawapo ya mbinu za mawasiliano iliyotumika kuhamasisha umma kuhusu masuala ya afya. Mabango mengi hutumia ishara na alama zinazotarajiwa kufasiriwa na hadhira ili kupata maana kamili. Uchunguzi ulilenga kubaini namna hadhira hufasiri ujumbe uliokusudiwa ili kubaini changamoto za kimawasiliano na kupendekeza njia za kuboresha mawasiliano haya. Nadharia ya Uhusiano iliyoasisiwa na Sperber & Wilson (1986) na kuendelezwa na Clark (2013) ndiyo iliyoongoza uchunguzi huu. Muundo wa utafiti huu ni wa mseto. Eneo la utafiti lilikuwa Kaunti ya Kakamega. Utafiti ulilenga wauguzi, wagonjwa na walezi wao waliozuru vituo vya afya vya kiwango cha pili vya serikali, pia ulilenga mabango ya afya yaliyoandikwa katika lugha ya Kiswahili katika vituo hivi. Makala ilibaini kuwa japo zaidi ya nusu ya wasailiwa walielewa ujumbe uliokusudiwa, sehemu kubwa ya hadhira haikufasiri mabango ipasavyo, jambo linaloashiria kuwepo kwa changamoto katika uwasilishaji au uelewekaji wa ujumbe. Baadhi ya sababu zilizochangia hali hii ni kuwa wasailiwa hawakuhusisha muktadha na maarifa ya awali katika fasiri. Utafiti unahitimisha kuwa changamoto za mawasiliano ya afya kupitia mabango huenda ni mojawapo ya sababu za maenezi ya magonjwa. Ufanisi wa mabango haupo tu katika uwepo wake, bali pia katika namna ujumbe unavyopokelewa na kufasiriwa na hadhira. Hivyo, inapendekezwa kuwa wabunifu wa mabango watumie lugha na ishara zilizorahisi kueleweka. Wazingatie kwa kina muktadha wa hadhira ili kuboresha uelewa na kupunguza fasiri potofu. Inatarajiwa kuwa, kazi hii itawafaidi wabunifu wa mabango ya afya na wataalamu wa mawasiliano ya afya kuboresha sera na mipango ya afya ya umma.
Keywords
Article Details
Copyright (c) 2026 Alice Khayali, Deborah Amukowa

This work is licensed under a Creative Commons Attribution-NonCommercial-ShareAlike 4.0 International License.
